Wednesday, 5 June 2013

MAKALA: NI UPUUZI KUMSHUSHA THAMANI, KUMUACHA JUMA KASEJA - SIMBA IIGE MFANO WA YANGA KWA NSAJIGWA - MAN U NA GIGGS





KLABU ya soka ya Simba haikuweza kufanya vizuri msimu uliopita katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara, kwani kutoka bingwa mtetezi iliambulia nafasi ya tatu msimu uliopita na kuiacha Yanga ikitwaa ubingwa. 
Hadi kutwaa nafasi ya tatu, Simba ilipambana vilivyo kwani Kagera Sugar nayo ilikuwa ikiwania nafasi hiyo kwa udi na uvumba. Jitihada za wachezaji na benchi la ufundi ndizo zilizoifanya Simba kutwaa nafasi ya tatu.
Usajili ukiwa unaendelea, Simba imeshamsajili kipa Andrew Ntala kutoka Kagera Sugar, huku tayari ikiwa na makipa Juma Kaseja na Abel Dhaira. Usisahau yule wa kikosi cha pili cha timu hiyo.
Wakati Simba ikilundika makipa hao, mkongwe Kaseja ni kama hatakiwi tena na timu hiyo, kwani kitendo cha kumsajili kipa namba moja wa Kagera, Ntala huku Dhaira akiwepo kikosini inaonyesha wazi mmoja kati ya Kaseja au Dhaira anatakiwa kuondoka.
Dhaira hadi anatua Simba alikuwa kipa wa kutegemewa wa timu ya taifa ya Uganda, The Cranes, hata huyu Ntala naye ni tegemeo la Kagera. Hii ina maana wote hao sasa wanatakiwa kupambana na Kaseja kuwania nafasi ya kwanza kikosini.
Ni ngumu kwa Simba kuachana na Dhaira kwani mkataba wake ni mkubwa na ambao unaweza kuigharimu Simba kiasi kikubwa cha fedha kuuvunja.
Popote pale duniani, huwezi kusajili makipa namba moja wawili kutoka timu nyingine huku tayari ukiwa na kipa hodari. Hii ni sawa na usajili mwingine wa nafasi nyingine uwanjani.
Tayari kuna tetesi kwamba, Simba ipo tayari kumwachia Kaseja ajiunge na klabu nyingine kwa madai ya kushuka kiwango na kushindwa kuisaidia timu kushika moja kati ya nafasi mbili za juu.
Mchakato mzima wa kuhakikisha Kaseja anaondoka Simba unaongozwa na kiongozi mmoja ambaye sasa ana sauti ndani ya klabu hiyo na mbaya zaidi hakuna sababu za msingi za kumuacha Kaseja.
KUSHINDWA KUISAIDIA SIMBA
Sababu kwamba Kaseja ameshindwa kuisaidia Simba haingii akilini kutokana na ukweli kwamba hata katika mechi ambazo Simba imefungwa Kaseja akiwa langoni, kuna vitu vingi vilikuwa vinatokea.
Hadi sasa hakuna hoja ya msingi iliyotolewa na uongozi juu ya mpango huo unaotengenezwa wa kuhakikisha Kaseja anaondoka Simba kwa njia yoyote ile, bali inayolazimishwa ni hii ya kushindwa kuisaidia timu.
Hawafafanui jinsi kipa huyu alivyoshindwa kuisaidia Simba kushika moja kati ya nafasi mbili za juu, kwani hajawahi kufungwa mabao manne katika mechi moja na idadi kubwa ya kufungwa kwake katika mchezo mmoja haizidi mabao matatu.

No comments:

Post a Comment